IQNA

Nchi za Kiarabu kukutana kikao cha dharura kujadili kadhia ya Quds

15:20 - May 09, 2021
Habari ID: 3473893
TEHRAN (IQNA)- Jumuiya ya nchi za Kiarabu (Arab League) imeamua kuitisha kikao cha dharura kwa lengo la kuchukua maamuzi kuhusu jinai za utawala wa Kizayuni wa Israel kufuatia ombi la Mamlaka ya Ndani ya Palestina.

Kwa mujibu wa taarifa Arab League imetangaza kuwa kesho Jumatatu itaitisha kikao cha dharura cha kuchukua maamuzi kuhusu njia za kukabiliana na jinai za israel huko Quds, baada ya Mamlaka ya Ndani ya Palestina kuwasilisha ombi rasmi la kuitishwa kikao hicho.

Kabla ya hapo, Riyadh al Maliki, Waziri wa Mambo ya Nje wa Mamlaka ya Ndani ya Palestina alitaka kuitishwe vikao vya dharura vya taasisi na vyombo mbalimbali vya kimataifa kwa shabaha ya kuwaunga mkono Wapalestina mbele ya jinai za Wazayuni.

Riyadh al Maliki alisema amewasiliana na mabalozi wa Palestina nje ya nchi katika mkakati wa kuitishwa mikutano ya dharura ya kimataifa ya Jumuiya ya Nchi za Kiarabu, Jumuiya ya Ushirikiano wa Kiislamu (OIC), Baraza la Haki za Binadamu la Umoja wa Mataifa na Baraza la Usalama la umoja huo.

Al Maliki aliongeza kuwa, Mamlaka ya Ndani ya Palestina inafanya jitihada za kuhakikisha kwamba, mikutano ya jumuiya hizo inatoa taarifa zinazolaani jinai na uhalifu unaondelea kufanywa na Israel na kuzihimiza nchi mbalimbali zikate uhusiano wao na utawala huo wa ubaguzi wa rangi kwa sababu ya kutenda jinai dhidi ya binadamu.

Ijumaa ya mwisho ya Mwezi Mtukufu wa Ramadhani ambayo pia ilikuwa Siku ya Kimataifa ya Quds ilishuhudia hujuma mpya askari wa utawala haramu wa Israel dhidi ya Msikiti Mtakatifu wa Al Aqsa mjini Quds.

3970171

captcha