IQNA

Watetezi wa haki za binadamu wataka Israel ichukuliwe hatua kwa kumuua Shireen Abu Aqleh

22:02 - May 13, 2022
Habari ID: 3475245
TEHRAN (IQNA)- Mashirika na makundi 250 ya kutetea haki za binadamu yametoa wito wa kuchukuliwa hatua za kisheria utawala haramu wa Israel kwa jinai uliyotenda ya kumuua mwandishi habari wa Televisheni ya al-Jazeera Shireen Abu Aqleh.

Taarifa ya pamoja ya asasi na mashirika hayo ya kutetea haki za binadamu imelaani vikali jinai hiyo ya Israel na kueleza kwamba, kuna haja kwa utawala huo ghasibu kuchukuliwa hatua kwa jinai yake hiyo.

Sehemu nyingine ya taarifa hiyo imeeleza kuwa, jinai hiyo ya Israel ya kumuua kwa kumpiga risasi mwandishi habari Shireen Abu Aqleh ni natija ya kimya cha jamii ya kimataifa kwa jinai za kila leo za utawala huo ghasibu dhidi ya wananchi wa Palestina.

Taarifa hiyo imekosoa vikali pia undumakuwili wa jamii ya kimataifa kuhusiana na masuala mbalimbali likiiiwemo suala la haki za binadamu.

Mapema Jumatano, mwandishi wa habari ya televisheni ya al Jazeera, Shireen Abu Akleh, 51, alipigwa risasi na kuuliwa shahidi kikatili na wanajeshi wa utawala wa Kizayuni wa Israel wakati akiwa kwenye kazi yake ya kuripoti uvamizi wa kijeshi wa jeshi la Israel katika kambi ya wakimbizi wa Palestina ya Jenin.

Jinai hiyo inaendelea kulaaniwa kimataifa huku watetezi wa haki za binadamu wakitaka utawala huo wa Kizayuni ufikishwe kizimbani.

Jeshi la utawala wa Kizayuni limekiri baada ya kufanyika uchunguzi kuwa, Shireen Abu Aqleh aliuliwa kwa kupigwa risasi na wanajeshi wa utawala huo.

4056606

captcha