Akizungumza leo katika ufunguzi wa 'Kongamano la Kimataifa la Kupambana na Misimamo Mikali ya Kidini' katika mji mkuu wa Misri, Sheikh Ahmed al Tayeb amelaani vikali 'jinai za kinyama' zinazofanywa na kundi la kigaidi la Daesh nchini Iraq na Syria. Mwanazuoni huyo wa ngazi za juu wa Kisuni amesema magaidi wa Kitakfiri wanaeneza taswira potofu kuhusu Uislamu duniani. Ameongeza kuwa "wakitumia bendera ya dini tukufu ya Kiislamu, wamejippaciha jina la 'Dola la Kiislamu' katika njama zao za kueneza Uislamu bandia." Sheikh Al Tayeb amezungumzia pia sababu za kidini, kisiasa na kiuchumi za kuibuka makundi ya kigaidi katika nchi za Kiislamu. Amesema wanazuoni wa Kiislamu nao pia wanabeba lawama kutokana na kutotekeleza majukumu yao na hivyo kupelekea kuibuka misimamo mikali ya kidini na makundi ya kigaidi kama al-Qaeda. Akiashiria madai ya Marekani kuwa imeunda muungano wa kukabiliana na makundi ya Kitakfiri Iraq na Syria, Sheikh Al Tayeb amesema, Marekani inapaswa kukabiliana na nchi ambazo zinaunga mkono magaidi kifedha na kijeshi.
Wanazuoni kutoka nchi kadhaa zikiwemo Jamhuri ya Kiislamu ya Iran, Saudi Arabia na Morocco wanashiriki katika mkutano huo ulioandaliwa na Chuo Kikuu cha Al Azhar.../mh