IQNA

Msikiti wahujumiwa Ujerumani mara mbili katika kipindi cha wiki mbili

22:09 - January 02, 2021
Habari ID: 3473518
TEHRAN (IQNA)- Msikiti mmoja umehujumiwa katika mji wa Baden-Wurttemberg kusini magharibi mwa Ujerumani mara mbili katika kipindi cha wiki mbili.

Mapmea Ijumaa, Januari Mosi, Msikiti wa Fatih katika mji wa Sontheim ulishambuliwa na hasara kusababishwa, amesema Ali Ozdemir, mwenyekiti wa kamati ya msikiti huo.

Kwa mujibu wa taarifa, msikiti huo ambao unasimamiwa na Jumuiya ya Waislamu Waturuki, DITIB, uliharibiwa moja ya madirisha yake katika hujuma hiyo.

Ozdemir amesema shambulizi hilo lilikuwa la pili katika kipindi cha wiki mbili dhidi ya msikiti huo jambo ambalo limepelekea Waislamu wanaoswali hapo kuingiwa na wasiwasi.

Aidha amesema maafisa wa polisi katika eneo hilo wameanzisha uchunguzi. Katika hujuma ya awali watu wasiojulikana walichora alama ya msalaba katika ukuta wa msikiti huo.

Ujerumani imeshuhudia ongezeko la chuki dhidi ya Waislamu na wahamiaji katika miaka ya hivi karibuni, chuki ambazo zinachochewa na vyama vya mrengo wa kulia vyenye misimamo ya kuvurutu ada dhidi ya watu wasiokuwa Wajerumani asili.

Ujerumani ni nchi yenye idadi ya watu zaidi ya milioni 81 na ina Waislamu takribani milioni tano na hivyo kuifanya nchi ya pili kwa idadi ya Waislamu Ulaya Magharibi baada ya Ufaransa. Aghalabu ya Waislamu Ujerumani wana asili ya Uturuki.

Mwaka jana polisi nchini Ujerumani waliwakamata watu 12 ambao walishukiwa kuanzisha mtandano wa mrengo wa kulia wenye misimamo mikali kwa lengo la kutekeleza hujuma dhidi ya wanasiasa, wakimbizi na Waislamu.

Idara ya Usalama wa Taifa Ujerumani inaamini kuwa kuna karibu watu 24,100 wenye misimamo mikali ya mrengo wa kulia ya kufurutu ada na karibu nusu yao wako tayari kutumia mabavu na kutekeleza hujuma za kigaidi dhidi ya wakimbizi, raia wa kigeni, Waislamu na wanasiasa wasioafikiana na sera za mrengo huo wa kulia.

3473572/

captcha