Kanisa Katoliki Austria lalaani mpango wa serikali dhidi ya Waislamu
TEHRAN (IQNA)- Kiongozi wa kanisa Katoliki nchini Austria amelaani vikali hatua ya serikali ya nchi hiyo kuzindua kile ambacho kimetajwa kuwa ni ‘Ramani ya Uislamu” kwa lengo la kuwabana Waislamu.
Katika taarifa, kiongozi wa Kanisa Katoliki Austria Kadinali Christoph Schoenborn amesema kuzinduliwa ramani hiyo ni jambo linalotia wasiwasi na ni hatua isiyosaidia kuleta uthabiti katika jamii.
Hivi karibuni serikali ya Kansela Sebastian Kurz wa Austria ilizindua "Ramani ya Uislamu " iliyozusha utata mkubwa. Kadinali Schoenborn, amesema ni ‘hatari kueneza dhana kuwa jamii moja ya kidini inashukiwa kwa ujumla.
Waziri wa Utangamano wa Austria, Susanne Raab alizindua tovuti inayoitwa Ramani ya Kitaifa ya Uislamu, ambayo ina majina na maeneo ya misikiti, jumuiya, na maafisa zaidi ya 620 Waislamu na mawasiliano yao nje ya nchi.
Taarifa hiyo imesema: "Ni muhimu kwa Austria kuacha kulenga wahamiaji na Waislamu kwa kuwatia "alama", na badala yake itekeleze sera za kuwajibika".
Askofu wa Kiinjili wa Kilutheri wa Ujerumani, Michael Chalupka naye pia ameeleza wasiwasi wake kuhusiana na hatua hiyo na amemtaka Raab aondoe tovuti hiyo.
Austria inakosolewa kwa kugeuka na kuwa kituo cha sera za chuki dhidi ya Uislamu barani Ulaya.