Mtu anaweza kuwa na biashara za aina mbili, moja ni biashara ya kidunia na watu wengine na nyingine ni biashara ya kiroho na Mungu. Katika biashara ya kiroho, mtu hutoa sadaka au kukopesha pesa kwa wale wanaohitaji. Matokeo yake yatadhihirika sio tu huko Akhera bali hata duniani kupitia kuongezeka kwa Rizq (riziki) na mali.
Hivyo mtu asifikiri amepata hasara katika biashara yake na Mwenyezi Mungu. Inaweza kuonekana hivyo juu juu, lakini kwa kweli inafunuliwa kwamba faida halisi ni ya wale wanaofanya biashara na Mungu.
Kufanya biashara na Mwenyezi Mungu katika mfumo wa Infaq (sadaka) ni biashara isiyo na hasara na faida nyingi.
Mwenyezi Mungu anasema katika aya ya 29 ya Suratul Fatir:" Hakika wale wanao soma Kitabu cha Mwenyezi Mungu, na wakashika Sala, na wakatoa kwa siri na kwa dhaahiri katika tulivyo waruzuku, hao hutaraji biashara isiyo bwaga."
Biashara hiyo ya kiroho na kujitolea mali na maisha ya mtu katika njia ya Mwenyezi Mungu humwokoa mtu kutokana na mateso katika dunia hii na ijayo na kumpeleka kwenye pepo na wokovu wa milele:
“ Enyi mlio amini! Nikuonyesheni biashara itakayo kuokoeni na adhabu iliyo chungu? Muaminini Mwenyezi Mungu na Mtume wake, na piganeni Jihadi katika Njia ya Mwenyezi Mungu kwa mali yenu na nafsi zenu. Haya ni bora kwenu, ikiwa nyinyi mnajua. Atakusameheni dhambi zenu, na atakutieni katika Mabustani yapitiwayo na mito kati yake, na maskani nzuri nzuri katika Bustani za milele. Huko ndio kufuzu kukubwa." (Suuratul Ass'af Aya ya 10 -12)
Kwa hivyo mtu anapaswa kuwa mwangalifu na nani anafanya biashara. Mfanyabiashara mwenye busara ni yule anayefanya biashara na mtu ambaye anapata faida kubwa zaidi.
Kufanya biashara na Mwenyezi Mungu kunahakikisha faida katika ulimwengu huu na ujao. Faida kidogo ya kidunia isitufanye tuache faida halisi, ambayo ni wokovu na furaha ya kudumu.
3480178