Kikosi hicho kipya ambacho kimepewa jina Tulkarm, kiko katika kambi ya wakimbizi ya Kipalestina katika mji wenye jina hilo hilo.
Kulingana na ripoti ya Jumatano ya mtandao wa habari wa Al-Alam, Brigedi ya Tulkarm itakuwa nyongeza ya Brigedi ya Al-Quds ambayo inafanya kazi katika Ukingo wa Magharibi unaokaliwa kwa mabavu, msemaji wa brigedi hiyo alisema, na kuongeza kuwa dhamira kuu ya kikosi hicho kipya itakuwa kuilinda Kambi ya Tulkarm dhidi ya uvamizi wa Israel.
"Kikosi cha Tulkarm kimeundwa kujibu uhalifu wa Wazayuni katika Kambi ya Tulkarm ... Tunawaambia wavamizi kuwa tuko tayari kujibu uchokozi wao," msemaji huyo alisema kwa sharti la kutotajwa jina.
Tulkarm iko kaskazini-magharibi mwa Ukingo wa Magharibi unaokaliwa kwa mabavu na kambi yake ya wakimbizi imeshuhudia ongezeko la mashambulizi ya wanajeshi wa Israel tangu mwaka jana.
Hayo yanajiri kama sehemu ya mwelekeo mkubwa wa mashambulizi ya vikosi vya Israel na walowezi dhidi ya Wapalestina katika Ukingo wa Magharibi unaokaliwa kwa mabavu katika kipindi cha miezi 16 iliyopita.
Sababu kuu ya kupamba moto kwa mapigano ni kuendelea kwa Israel ujenzi wa makazi haramu ya walowezi wa Kizayuni katika Ukingo wa Magharibi, eneo ambalo ililiteka na kukalia kimabavu baada ya vita vya mwaka 1967 na Waarabu.
Ghasia pia zimezidi kuwa mbaya katika ardhi za Palestina katika miezi ya hivi karibuni huku baraza la mawaziri lenye misimamo mikali ya mrengo wa kulia la Israel likiendelea kutekeleza hatua za uchochezi katika Msikiti wa al-Aqsa ulio katika mji wa Al Quds (Jerusalem), mji wa tatu kwa utakatifu katika Uislamu, hasa kwa kuruhusu Wazayuni wenye itikadi kali kuvamia eneo hilo la Kiislamu
Idadi ya Wapalestina ambao Israel imewaua shahidi katika ardhi za Palestina zinazokaliwa kwa mabavu na Gaza imepita 200 mwaka huu. Aghalabu ya vifo hivi vilitokea katika Ukingo wa Magharibi. Hii inafanya 2023 kuwa mwaka mbaya zaidi kwa Wapalestina katika Ukingo wa Magharibi tangu 2005, wakati Umoja wa Mataifa ulipoanza kurekodi vifo.
348525